Kenya Tue 09-12-2008
By a Correspondent
Fikiria mchoro wa rangi bila maumbo, mwangaza au kivuli. Mchoro huu hauvutii wala kupendeza. Hakika sio mchoro halisi. Hivyo ndivyo ulimwengu ungalikuwa bila watoto.
Na je chakula ambacho hakina chumvi wala bizari? Hakiliki, hakina ladha. Hii ni taswira ya maisha bila sanaa.
Fikiria ubora wa maisha yenye watoto wasanii... itawezekanaje? Nilizungumza na mwalimu wa shule ya wadudu - watoto wa umri wa miaka miwili hadi miaka sita - Bi. MaryAnne Marete ambaye ana tajriba ya miaka kumi, na alinidokezea yafuatayo.
Watoto hujifunza kupitia yale wanayoyaona na kuyahisi zaidi ya yale wanayoyasikia. Mandhari ya kwanza ya watoto kujifunza kuhusu maisha, ni nyumbani.
Vile vile somo lao la kwanza la sanaa. Ni jambo la rahisi. Kama mzazi, unapoanda chakula mezani, kwa mfano matunda, unaweza kuyapanga kwenye bakuli ama uteo kwa namna ya kuvutia.
Pia, hakikisha mapambo ya nyumba na samani ni ya kuvutia na kusisimua. Isitoshe, vyumba vya kulala vya watoto, vinafaa vikolezwe rangi nyekundu, manjano au samawati na vipambwe kwa vibonzo wanavyopenda.
Ikiwa unaishi katika nyumba ya kukodesha na huwezi kuzipaka kuta rangi nyingine, tumia pazia zenye rangi na michoro ya kuvutia. Sebuleni, picha zilizochorwa na watoto na zilizowekwa fremu zinaweza kuning’inizwa kutani. Hakuna himizo kubwa kwa usanii wa watoto kuliko hili.
Wakati wa mapumziko ndio bora zaidi kwa kukuza usanii. Ni vizuri kuwavumbulia watoto vifaa vya aina nyingi vinavyopatikana nyumbani, kwa mfano makaa, chaki, kalamu zenye rangi na za mate, rangi za maji, matope, ‘mishumaa’, na hata unga wa chapati.
Vyombo vya kupikia pia vyaweza kutumika kama vifaa vya kuchezea, lakini kwa idhini ya mlezi. Vifaa vyote hivi vinaweza kutumika kuunda maumbo kama ya watu, wanyama, magari, vifaa, nyumba na chochote kile kinachonasa fikira zao. Huu ndio mwelekezo thabiti katika kuchochea usanii.
Bila shaka msomaji waweza kuwa ukijiuliza kwa nini ninatilia mkazo uchocheaji wa usanii katika watoto. Utakubaliana nami kwamba watoto ni tumaini la jamii na hazina la utamaduni. Hivyo basi sanaa itaendelea na kuimarika zaidi ikiwa tutawaridhisha.
Sanaa pia ni njia ya kujieleza kibinafsi. Ni kioo la kuangazia nafsi na tajriba za mtoto, hisia zake, pamoja na miondoko yake ya kimwili.
Bila shaka, ukitaka kujua mitazamo yao ya jamii, chunguza michoro na rangi watoto wanazozitumia. Mathalan, mtoto anayemchora mamaye kama alama ya kituo na mwalimu wake kama kidude kikubwa, anathibitisha umuhimu wa mwalimu wake dhidi ya mzazi wake. Watoto wenye masaibu ya kinyumbani au wenye athari za kiwiliwili wanaweza kujieleza barabara kwa njia ya sanaa.
Tajriba wasizoweza kueleza au kufafanua hufichulika. Hasira na uchungu wa mtoto hubainika ikiwa ametapakaza rangi nyeusi ama nyekundu katika michoro yake. Sanaa inaweza kuwa njia mwafaka ya kutuliza hisia za kutatiza na kuelekeza nguvu na fikra za watoto.
Je, mtoto aliye na kipawa cha kipekee tutamtambuaje? Watoto kama hawa hubainika kwa umbuji walio nao. Katika uchoraji au uundaji hawatumii vifaa walivyozoea au kusomea peke yake, bali wao hutumia chochote kile kinachopatikana. Mtoto kama huyo, atachora akitumia vidole, viganja, kucha, nyao, nyuzi, miti, matawi na kadhalika.
Anapoangalia angani, haoni mawingu tu, bali maumbo kama ya ndovu, watu, na vidude vya kila aina. Kueua na kukuza kipawa hiki zaidi, ni muhimu kuwatembeza watoto kuvinjari mandhari, sokoni, maonyesho na mashindano ya kisanaa pamoja na kuwajuliza na watoto wa rika tofauti. Kuwahusisha katika michezo mbali mbali kama kuogelea, kandanda, mbio na nyinginezo huwasaidia katika umbuji.
Ni bora kuwatumbuiza watoto na muziki tofauti kwa sababu hisia zao huathirika kwa njia tofauti na wataibua sanaa za kila aina. Kwa ufupi, siri ya kuvumbua mtoto mwenye kipawa ni kwa kumwelekeza katika hali tofauti za kimaisha. Hata hivyo usimlazimishe mtoto.
Mhimize, msifu na umshauri kwa upole na ustadi. Kwa jumla, mwelekeo wa watoto ni wa matumaini na mafanikio. Ukiwahamasisha vilivyo, utastaajabu matokeo ya sasa na ya vizazi vijavyo.
Wasanii wenye uvumi na walio bingwa sio wa kuzaliwa tu, bali wanaweza kuibuka kwa watoto waliolelewa katika usanii. Msanii Jak Katarikawe – mzaliwa Uganda anayeishi Kenya – ambaye ana maonyesho ya michoro yake katika jumba kuukuu la mkuu wa mkoa wa Nairobi, alijifunza usanii kwa kumuiga mama yake, aliyependa kupamba nyumba yake kwa michoro.
Jitihada unazozifanya wakati huu nyumbani mwako, zinaweza kuchangia kwa kumfanya mwanao msanii mashuhuri katika siku za usoni.
Artists Portfolios
Editorials By Regions
Featured Artist Portfolio
Title: Untitled 4
Name: Eria Nsubuga
Country: Uganda 
Medium: Acrylic
Size: 79cmx60cm
Click here to view
News
Features
Editorials
News From External Sources







skip
to top
Cameroon
Tanzania
Angola
South Africa
Zimbabwe
Senegal
International